HABARI

Wizara Ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Yatekeleza Agizo La Rais Magufuli Kabla Ya Siku 7

Waziri  wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Kamwelwe, amezindua rasmi magari kupita katika daraja la Kiyegeya la mchepuko lililopo Wilaya ya Kilosa katika barabara ya Morogoro- Dodoma kabla ya siku saba zilizoagizwa na Rais John Magufuli.
Agizo la Rais Magufuli lilitolewa Machi 16 mwaka huu, wakati akiwa kwenye daraja hilo na kubaini kuwapo kwa uzembe katika usimamizi wa ujenzi wake na kutoa siku saba kwa waziri na watendaji wake kukamilisha daraja la mchepuko na magari kupita haraka, huku akisisitiza asisikie magari yamekwama katika eneo hilo.
Kukamilika kwa muda mwafaka kwa ujenzi wa daraja hilo umechangiwa na uamuzi wa wizara hiyo kununua makalvati makubwa 120 ya zege kutoka Kampuni ya Yapi Merkezi ya Uturuki inayojenga mradi wa reli ya kisasa (SGR) kutoka Dar es Salaam -Makutupora.
Akizungumza wakati wa kuanza kupita kwa magari ya kwanza ya majaribio, Waziri Kamwelwe alisema daraja hilo la mchepuko lina upana wa mita tisa, ambalo lina uwezo wa kupitisha magari makubwa mawili.

“Niliamua kuitumia gari langu liwe ofisi ya muda, tulikaa mimi mwenyewe, Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi, Elius Mwakalinga na Mtendaji Mkuu wa Tanroads, Mhandisi Patrick Mfugale na kuja na mwafaka wa kununua makalvati makubwa ya zege 120 kutoka Reli ya SGR,” alisema Waziri Kamwelwe.

Alisema daraja hilo kuwa na uwezo huo wa kupitisha magari hayo mawili kwa mara moja, lakini kwa sehemu iliyozinduliwa litaruhusiwa kupita gari moja kwa zamu ili kuruhusu kuendelea ujenzi mwingine wa kuunganisha daraja lingine lenye upana kama huo liendelee.

“Kama mlivyosikia mimi na wenzangu tulipewa siku saba na Rais Dk. Magufuli tuwe tumekamilisha kujenga daraja la muda la mchepuko, na wizara imekamilisha ujenzi wa daraja hilo ndani ya muda wa siku sita, na hivi sasa nazindua rasmi kuanza kupita magari,” alisema Waziri Kamwelwe.

Akizungumzia kuhusu ujenzi wa daraja lingine ambalo lina upana kama huo litakalounganishwa na lilokamilika, alisema lengo lake litakapokamilika kuwezesha kupita magari hayo kwa nafasi zaidi kila upande katika daraja hilo.
Hata hivyo, Waziri huyo hakuwa tayari kutaja gharama ya ununuzi wa makalvati hayo, na kueleza kila kalvati moja lina urefu wa mita mbili na uzito wa tani 13 na mpaka kukamilika hatua ya pili yatatumika jumla makalvati 120.

“Njia hii ya mchepuko sasa itakuwa ni ya kudumu kwa magari kupita pande zote mbili bila ya kusubiri kwa zamu,” alisema Waziri Kamwelwe.

About the author

kidevu

Leave a Comment