HABARI

MUANGOLA WA YANGA AWEKA REKODI YAKE KWA MKAPA

 

KIUNGO mshambuliaji wa Yanga, Carlos Carlinhos, raia wa Angola, amehusika katika mabao matano katika michezo 6 pekee aliyoicheza Yanga katika ligi kuu msimu huu.

 

Mchezaji huyo tangu asajiliwe na Yanga katika dirisha kubwa, ameshindwa kucheza michezo mingi kutokana na majeraha ya mara kwa mara ambayo yamekuwa yakimsumbua.

 

 Carlinhos aliifungia Yanga bao katika ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Mtibwa katika mchezo uliochezwa Uwanja wa Mkapa jijini Dar, akipokea pasi kutoka kwa Tuisila Kisinda na kufikisha bao lake la tatu ndani ya ligi.

 

 Katika mchezo huo Carlinhos aliingia katika dakika ya 70 akichukua nafasi ya Ditram Nchimbi ambapo ilimchukua dakika 2 tu mchezaji huyo kuifungia Yanga bao ambalo lilidumu mpaka mpira unamalizika jambo lililomfanya aweze kuweka rekodi ya kutumia muda mfupi kuipa pointi tatu timu yake.

 

 

Sasa kiungo huyo anakuwa amefikisha mabao matatu na asisti mbili katika michezo sita ya ligi kuu ambayo ameichezea klabu hiyo tangu asajiliwe katika dirisha kubwa la usajili.


Timu yake ipo nafasi ya kwanza ikiwa na pointi 49 baada ya kucheza mechi 21 ndani ya ligi.

 

 

Aidha, pasi mbili za mabao za Carlinhos alizozitoa ilikuwa katika michezo dhidi ya Mbeya City katika ushindi wa Yanga wa bao 1-0 akitoa asisti kwa Lamine Moro, pasi nyingine ilikuwa katika ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Mtibwa Sugar ugenini akitoa pasi kwa Lamine Moro.

 

 

Katika upande wa mabao kiungo huyo alifunga katika mchezo dhidi ya Coastal Union Yanga ikishinda mabao 3-1, dhidi ya Namungo katika sare ya bao 1-1 na katika mchezo wa juzi dhidi ya Mtibwa, Yanga ikishinda kwa bao 1-0.

 

 

Kwa takwimu hizo ni wazi kuwa mchezaji huyo amekuwa hatari zaidi pindi anapopewa nafasi ya kucheza kwani katika michezo sita aliyocheza, amechangia idadi ya mabao matano.

About the author

kidevu

Leave a Comment