HABARI

YANGA YAPATA PRESHA, KISA KASI YA SIMBA NDANI YA LIGI KUU BARA

 


 KOCHA Mkuu wa Yanga, Mrundi, Cedric Kaze amefi chua kuwa kwa sasa wamekuwa kwenye presha kubwa ya kuhakikisha wanapata matokeo katika kila mchezo kutokana na kasi ya wapinzani wao wakiwemo Simba kuelekea kwenye mbio za ubingwa wa Ligi Kuu Bara msimu huu.

 

Kaze ametoa kauli hiyo ikiwa Yanga inaongoza ligi kwa pointi 49, ikifuatiwa na Simba wenye pointi 42 huku wakifuatiwa na Azam wakiwa na pointi 36.


Yanga imecheza jumla ya mechi 21 ndani ya Ligi Kuu Bara sawa na Azam FC inayonolewa na George Lwandamina huku Simba ikiwa imecheza jumla ya mechi 18 msimu wa 2020/21.


Mkononi imebakiwa na mechi moja ya kiporo cha mzunguko wa kwanza dhidi ya Namungo FC ambayo leo inacheza mchezo wa Kombe la Shirikisho dhidi ya 1 de Agosto ya Angola, Uwanja wa Azam Complex.


Kaze amesema kuwa matokeo wanayopata kwa sasa yamekuwa yakiongeza presha kwao lakini wataendelea kupambana kwa kuhakikisha wanafikia malengo.


“Hatujawa kwenye kipindi kizuri kwa sasa hasa upande wa matokeo, presha imekuwa kubwa upande wetu kwa sababu kila aliyekuwa nje anataka kuona matokeo mazuri na hilo ndiyo lengo letu kuona tunafanya hivyo.

 

“Kikubwa tunachokiangalia ni malengo ya timu kuweza kufikiwa kwa pamoja na kuweza kuondoa presha ambayo tumekuwa nayo kwa sasa kutokana na matokeo ya mechi ambazo zimepita na kasi kubwa ambayo wamekuwa nayo wapinzani (Simba), wetu ambao wamekuwa wakishinda michezo yao mfululizo,” amesema Kaze.


Kwenye mzunguko wa pili Kaze alikiongoza kikosi chake kwenye mechi mbili mfululizo ambapo aliambulia pointi mbili kati ya sita ambazo alikuwa anasaka.


Sare ya kufungana bao 1-1 dhidi ya Mbeya City na sare ya kufungana mabao 3-3 dhidi ya Kagera Sugar, aliibuka na ushindi kwenye mchezo dhidi ya Mtibwa Sugar kwa bao 1-0 lililopachikwa na Carlos Carlinhos, mwenye mabao matatu ndani ya ligi.

About the author

kidevu

Leave a Comment